JAPAN KUPITIA SHIRIKA LAKE LA JICA YATOA BILIONI 354.45 KUSAIDIA WAKULIMA- BENKI YA TADB KUZISIMAMIA - UMOJA BANKING BLOG

Breaking

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, 15 January 2025

JAPAN KUPITIA SHIRIKA LAKE LA JICA YATOA BILIONI 354.45 KUSAIDIA WAKULIMA- BENKI YA TADB KUZISIMAMIA

Waziri wa Fedha Dkt. Mwigulu Nchemba na Balozi wa Japan nchini Tanzania  Yasushi Misawa wakitia saini mkataba wa Sh. Bilioni 354.45 kwa ajili ya kusaidia wakulima katika hafla iliyofanyika Januari 14, 2025 jijini Dar es Salaam.

.....................................................

Na Dotto Mwaibale, Dar es Salaam


 SERIKALI  ya Japan kupitia Shirika lake la Maendeleo (JICA) imetoa Sh. Bilioni 354.45 kugharamia utelelezaji wa mradi wa Kilimo na Maendeleo Vijijini (Agriculture and Rural Development Two Step Loan) ukiwa na lengo la kuwanufaisha moja kwa moja wakulima kupitia mikopo midogo midogo.


Tayari Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Japan jana Januari 14, 2025 zimetia saini mkataba huo umesainiwa na Waziri wa Fedha Dkt. Mwigulu Nchemba na Balozi wa Japan nchini Tanzania Yasushi Misawa huku ikishuhudiwa na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Japan Hiyasuki Fuji.


Fedha hizo zilizotolewa kwa Tanzania kwa mfumo wa mkopo wa masharti nafuu na Serikali ya Japan kupitia Shirika lake la maendeleo (JICA) kinalenga kuwezesha vyama, vikundi vya wakulima na mkulima mmoja mmoja kupata mikopo ya muda mfupi, wa kati na mrefu kwa mazao ya ngano, mahindi, mpunga, alizeti na kilimo cha bustani.


Waziri wa Fedha Dkt. Mwigulu Nchemba akizungumza kwenye hafla ya utiaji saini wa mkata huo alisema  kupatikana kwa fedha hizo kunatokana na kazi nzuri inayofanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuendelea kuimarisha ushirikiano wa kidiplomasia na kiuchumi kati ya Tanzania na Japan.


Katika kipindi cha miaka mitatu ya hivi karibuni Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amefanya kazi kubwa ya kuifungua nchi kwa kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia na uchumi.


Alisema fedha hizo zinakwenda moja kwa moja kwa wakulima ili zikaongeze kasi ya mapinduzi kwenye sekta ya kilimo katika kuongeza uzalishaji, ubora na  thamani ya mazao. 


Kwa upande wake Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Japan Fuji alisema kuwa kiasi hicho cha fedha za mkopo wa masharti nafuu kimetolewa kuunga mkono dhamira na juhudi za Serikali ya Tanzania ya kuwakomboa wakulima kiuchumi.


“Tunatambua kazi nzuri inayoendelea kufanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuendeleza sekta ya kilimo. Japan tunaamini kiasi hiki cha fedha kitaenda kuongeza kasi ya kuiboresha sekta ya kilimo ili iweze kuwaongezea kipato wakulima na kuwatoa katika umaskini”. alisema Waziri Fuji.


Naye Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki. Cosato Chumi ambaye alimwakilisha Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo katika hafla hiyo, alieleza kuhusu namna utekelezaji wa diplomasia ya uchumi chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan unavyovutia wadau wa maendeleo kusaidia katika sekta mbalimbali nchini.


“Mambo haya mazuri tunayoyashuhudia leo ni matokeo ya juhudi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan za kuifungua nchi kwa kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia na Jumuiya ya Kimataifa, ni wajibu wetu kuendelea kumuunga mkono Rais wetu kwenye utekelezaji wa diplomasia ili aendelee kuleta maendeleo nchini”.  alisema Chumi.


Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB), Frank Nyabundege alisema mafanikio hayo katika sekta ya kilimo yanatoka na kazi nzuri ya Rais Dkt. Samia Suluhu anayoifanya ya kuingunisha Tanzania na mataifa mengine kidipromasia na kufungua fursa za kilimo huku lengo lake likiwa watanzania watoke kwenye kilimo cha kawaida na kuingia katika kilimo biashara.


Alisema fedha hizo zitakopeshwa kwa wakulima kwa riba ndogo na kwa muda mrefu na kueleza kuwa kutokana na kazi kubwa inayofanywa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kilimo kimendelea kuwa cha tija ambapo mwaka juzi nchi iliweza kupata tani zaidi ya Milioni 18 za nafaka na mwaka jana zikapanda hadi kufikia tani zaidi ya Milioni 20.


Mkataba huo utasimamiwa na JICA kwa niaba ya Serikali ya Japan na kwa upande wa Serikali ya Tanzania utatekelezwa na Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB). 

Waziri wa Fedha Dkt. Mwigulu Nchemba na Balozi wa Japan nchini Tanzania Yasushi Misawa wakionesha mkataba wa shilingi bilioni 354.45 uliosaniwa kwa lengo la kusaidia wakulima kupitia mikopo. 

Waziri wa Fedha Dkt. Mwigulu Nchemba na na Makamu wa Rais wa Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Japan (JICA), Bi. Miyazaki Katsura, wakionesha hati za mkataba huo.
Waziri wa Fedha Dkt. Mwigulu Nchemba akizungumza katika hafla hiyo.
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Japan Hiyasuki Fuji akizungumza. 
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Cosato Chumi akizungumza.
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB), Frank Nyabundege  akizungumzia kuhusu manufaa ya mkopo huo.
Wawakirishi kutoka Japan wakiwa kwenye hafla hiyo.
Waziri wa Fedha Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba na Makamu wa Rais wa Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Japan (JICA), Bi. Miyazaki Katsura, wakibadilishana hati za mkataba huo.
 

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad

Pages