MBUNGE wa Jimbo la Singida Mashariki Miraji Mtaturu ameunga mkono jitihada za Rais Samia Suluhu Hassan za kuwataka watanzania ambao watakuwa na uwezo wa kuwaleta wawekezaji nchini kufanya hivyo.
Mtaturu kwa kuona nia hiyo njema ya Rais Samia Suluhu Hassan leo Agosti 9, 2024 amewapokea Wawekezaji kutoka Kampuni ya ANHF & Kubena Gold Mines Limited ofisini kwake Ikungi na kufanya nao mazungumzo nao.
Akizungumza na waandishi wa habari alisema wawekezaji hao tayari amewaunganisha na wachimbaji wadogo wa Jimbo la Singida Mashariki ili wawasaidie kupata zana bora za uchimbaji, utaalam na mitaji ili kurahisisha kazi yao iwe na tija na kuweza kukuza uchumi wao na Taifa kwa ujumla.
“Nimewiwa kuunga mkono jitihada za Mhe. Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan za kuwataka watanzania wenye uwezo wa kuwaleta wawekezaji kuja kuwekeza nchini wafanye hivyo na ndio maana nikazungumza na hawa wenzetu kutoka India ambao wamefika leo hapa ofisini kwangu,” alisema Mtaturu.
Alisema moja ya jambo ambalo amewaambia wawekezaji hao ni kuwa Serikali ina wathamini wawekezaji na imeweka mazingira mazuri ya kazi na amewahakikishia kuwa watapewa ushirikiano muda wote watakaokuwepo hapa nchini.
Mkurugenzi wa Kampuni hiyo, Arfu Sheik ambaye aliongoza na viongozi wake waandamizi alitoa shukurani nyingi kwa Mbunge Mtaturu kwa mapokezi yake mazuri na nia yake njema ya kizalendo ya kuwasaidia wachimbaji ambapo ameahidi kuwasaidia wachimbaji hao ili waanze kufanya uchimbaji ulio na tija.
Kwa upande wake Katibu wa Wachimbaji wadogo Wilaya ya Ikungi (SIREMA) Wilaya ya Ikungi, Hamisi Nkingi akizungumza kwa niaba ya wachimbaji hao alimshukuru mbunge kwa kuwaunganisha na Mwekezaji ambaye ameonyesha nia ya kushirikiana nao na wameahidi kuwa waaminifu ili wafaidike na kazi yao ya uchimbaiji kwani changamoto kubwa waliyonayo ni zana duni za uchimbaji, utaalam na kutokuwa na mitaji ya uhakika.
No comments:
Post a Comment