Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Emmanuel Tutuba akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani)
...........................
Na John Buuku, Dodoma
SERIKALI kupitia Benki Kuu ya Tanzania (BoT) imesema itaendelea kusimamia
Benki zote nchini kwa kuzingatia viwango vya Kimataifa, huku wakitoa wito kwa
wananchi kujenga utamaduni wa kuhifadhi fedha benki kutokana uendeshaji wa
uchumi wa kisasa unategemea zaidi matuminzi ya utaratibu wa kibenki ambapo kwa
sasa umerahisishwa.
Akizungumza leo Agosti 7, 2024 katika Maonesho ya Kimataifa ya Kilimo
Nanenane yanayofanyika Nzuguni jijini Dodoma, Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania
(BoT) Bw. Emmanuel Tutuba, amesema kuwa ni muhimu kuhifadhi fedha benki kwani
ni sehemu salama.
“Ukitunza fedha nyumbani kuna athari nyingi zinazoweza kujitokeza ikiwemo
kuibiwa, kuungua moto, lakini ukitunza Benki na ikitokea changamoto yoyote
unarejeshewa fedha zako” amesema Gavana Tutuba.
Gavana Tutuba amesema kuwa BoT kupitia Bodi ya Bima ya Amana (DIB) wameweka
utaratibu mzuri wa kurejesha fedha za wateja kama ikitokea benki imefilisika.
“Benki ikifungwa serikali itahakikisha wateja wote waliojitokeza
watarejeshewa fedha zao kulingana na kiwango cha bima pamoja na kuwafatilia
wateja wote waliokopa ili waweze kurejesha madeni yao” amesema Gavana Tutuba.
Amesema kuwa DIB imeongeza kiasi cha kurudisha fedha kwa wateja kutoka milioni moja hadi milioni saba na Laki tano wakiwa na lengo la kulinda amana ya mteja.
Gavana Tutuba amefafanua kuwa kwa mujibu wa tathmini waliofanya mwezi june
mwaka huu inaonesha kuwa benki zote zina ukwasi pamoja na mitaji ya kutosha.
“Kiwango cha mikopo chechefu imeshuka hadi kufikia asilimia 4.3 ambacho ni
kiwango kipo chini na ukilinganisha na utaratibu wa kimataifa” alisema Gavana
Tutuba.
Katika hatua nyengine amewakumbusha watanzania ambao walikuwa wanahifadhi
fedha benki ambapo kwa sasa benki hiyo imefilisika kwenda Ofisi ya DIB kwa
ajili kuchukua fedha zao kama bado hawajachukua.
No comments:
Post a Comment