..............................
Imeandaliwa
na Dotto Mwaibale
(0754-362990)
AFISA wa Tanzania Commercial Bank (TCB), Ramadhani Kassim amesema mkulima mwenye uzoefu
kidogo wa kilimo akiwa na kitambulisho cha Taifa (NIDA) anaweza kukopeshwa
fedha na benki hiyo.
Kassim ameyasema hayo kwenye banda la benki
hiyo lililopo kwenye Maonesho ya saba (7) ya kitaifa ya mifuko ya programu za
uwezeshaji wananchi kiuchumi yaliyoandaliwa na Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (NEEC) yanayoendelea Uwanja wa Bombadia
mjini Singida.
“Benki yetu inahusika kuwasaidia wakulima kuwapatia
mitaji na mikopo ili waweze kufanya shughuli zao za kilimo popote pale nchini.
Alisema benki hiyo inawasaidia wakulima kwa
kuwapatia mikopo yenye riba nafuu baada ya kujaza fomu maalumu huku akiwa na
viambatanisho kama kitambulisho cha taifa, barua inayomtambulisha mtaa anaoishi
kutoka ofisi ya Serikali ya mtaa husika.
Aidha Kassim alisema ili mkulima aweze
kukopeshwa na benki hiyo sifa nyingine awe na uzoefu wa zao analolilima walau
kwa misimu miwili ili waweze kumfanyia utafiti kubaini mkopo ambao anaweza
kupewa kulingana na kilimo anacho kifanya.
Kassim alitumia nafasi hiyo kuwakaribisha
wakulima kutembelea banda lao lililopo kwenye maonyesho hayo kwa ajili ya
kupatiwa mkopo kwa wale ambao watakidhi vigezo.
No comments:
Post a Comment